KAMATI YA BUNGE YATOA MAAGIZO OSHA KUHUSU AFYA ZA WAFANYAKAZI

KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii imeutaka Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) kuweka utaratibu maalum wa kuwafuatilia wafanyakazi wanaobainika kuwa na changamoto za kiafya baada ya kufanyiwa uchunguzi, ili waweze kupata huduma na msaada unaostahili.

Agizo hilo limetolewa , Agosti 12, 2026, jijini Dodoma na Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Mhe. Hawa Mchafu katika kikao cha Kamati cha kupokea na kujadili taarifa ya utekelezaji wa shughuli za OSHA kwa mwaka wa fedha 2025/26.

Mhe. Mchafu amesema katika 2023/24, OSHA ilifanya uchunguzi wa afya kwa wafanyakazi 845, ambapo wafanyakazi 274 walibainika kuwa na magonjwa mbalimbali na kwamba takwimu hizo zinaonesha umuhimu wa kuwa na utaratibu endelevu wa kuwafuatilia wafanyakazi wanaobainika kuwa na changamoto za kiafya, badala ya kuishia katika hatua ya uchunguzi na kubaini matatizo pekee.

“Kamati inashauri kuwe na mfumo au utaratibu wa kufanya ufuatiliaji kwa wale wafanyakazi ambao watakuwa wamebainika kuwa na matatizo ya afya, ili waweze kufuatiliwa na kusaidiwa kutatuliwa changamoto zao,” amesema Mhe. Mchafu

Aidha, Kamati imeitaka OSHA kuendelea kutoa elimu kwa waajiri na wafanyakazi kuhusu usalama na afya mahali pa kazi, hususan kutokana na mabadiliko ya teknolojia yanayoendelea katika maeneo mbalimbali ya uzalishaji na utoaji huduma.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Deus Sangu, amesema usalama na afya mahali pa kazi ni msingi muhimu katika kujenga mazingira bora ya kazi na kuongeza tija kwa wafanyakazi.

“Ili tuweze kutimiza malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, tunahitaji nguvu kazi salama na yenye afya. Tunakupongeza Mwenyekiti na Kamati yako kwa kusimamia kwa karibu suala hili na kuendelea kutoa maelekezo ambayo yamekuwa na tija,” amesema Sangu.

Awali, akiwasilisha taarifa hiyo, Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Ajira na Mahusiano, Mhe. Dkt. Evaline Munisi, amesema utekelezaji wa sheria na kanuni za usalama na afya mahali pa kazi umeendelea kuleta matokeo chanya, ikiwamo kuongezeka kwa mwitikio wa waajiri kusajili maeneo yao ya kazi na OSHA.

Naye,  Mtendaji Mkuu wa OSHA, Khadija Mwenda, amewahakikishia wajumbe wa Kamati kuwa Wakala huo utaendelea kutoa elimu kwa wadau na kusimamia utekelezaji wa sheria ili kuhakikisha maeneo ya kazi yanakuwa salama, yenye afya na yanayochangia maendeleo endelevu ya uchumi wa taifa.

Post a Comment

0 Comments