Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi nchini, Jenerali Jacob John Mkunda, amewataka askari wapya waliohitimu mafunzo yao kukiishi kiapo cha utii wakati wote watakapokuwa wakitekeleza majukumu yao ndani ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania(JWTZ).
Aidha Jenerali Mkunda ametoa onyo kali kuwa jeshi halitasita kuchukua hatua za kisheria na kinidhamu dhidi ya askari yeyote atakayekwenda kinyume na kiapo hicho cha uaminifu kwa nchi na jeshi.
Wito huo ameutoa mkoani Pwani wakati wa hafla ya kufunga mafunzo ya awali ya kijeshi kwa kundi la 44 la mwaka 2025, yaliyofanyika katika Shule ya Mafunzo ya Awali ya Kijeshi, RTS Kihangaiko, iliyopo wilayani Bagamoyo. Katika hotuba yake, Jenerali Mkunda amewasisitiza wahitimu hao kuwa nidhamu na utii ndio msingi mkuu wa kazi ya kijeshi na bila hivyo hakuna usalama wa taifa.
Katika hatua nyingine, Mkuu huyo wa Majeshi amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Daktari Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuliwezesha jeshi kupata rasilimali na vifaa vinavyohitajika katika kuimarisha ulinzi wa mipaka ya nchi. Jenerali Mkunda amebainisha kuwa msaada wa Amiri Jeshi Mkuu umekuwa chachu ya mafanikio makubwa katika utendaji wa JWTZ.
Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Mafunzo ya Awali ya Kijeshi RTS Kihangaiko, Brigedia Jenerali Sijaona Michael Myala, amewapongeza askari hao kwa uvumilivu na jitihada walizozionyesha kipindi chote cha mafunzo.
Brigedia Jenerali Myala ameeleza kuwa mafunzo hayo yamewajengea vijana hao uzalendo wa hali ya juu na uwezo mkubwa wa kutekeleza majukumu ya jeshi kwa ufanisi, huku akibainisha kuwa wako tayari kuitumikia nchi kwa weledi.
Hafla hiyo ilihitimishwa kwa shamrashamra na maonesho mbalimbali ya kijeshi ikiwemo michezo ya kareti inayolenga kuimarisha ukakamavu, pamoja na burudani za muziki na ngoma za asili zilizowavutia waliohudhuria tukio hilo muhimu la kutaifisha askari hao wapya.


0 Comments